MREMA amtaja kortini mwakilishi wa Papa ilivyotumika kusambaza vipeperushi vya kumfanyia kampeni Mbatia

Shahidi wa kwanza katika kesi ya kupinga matokeo ya ubunge Jimbo la Vunjo, Augustine Mrema (TLP), ameieleza Mahakama jinsi siku ya ziara ya Balozi wa Baba Mtakatifu nchini, Askofu Mkuu Fransisco Padilla ilivyotumika kusambaza vipeperushi vya kumfanyia kampeni mbunge wa sasa, James Mbatia.

Mrema ambaye anapinga ushindi wa Mbatia, alitoa ushahidi wake mbele ya Jaji Lugano Mwandambo wakati akijibu maswali ya Wakili Mohamed Tibanyendera anayemtetea Mbatia.

Mwanasiasa huyo aliyegombea ubunge katika jimbo hilo alikana taarifa ya gazeti la Mwananchi la Februari 15, mwaka huu, lililomnukuu akisema kwamba hajutii kumpigia debe Rais John Magufuli wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana.

Katika gazeti hilo, Mrema alinukuliwa akisema pamoja na kutoswa ubunge bado anasimamia kwamba Rais Magufuli ndiye mtu aliyestahili kuongoza Tanzania.

Alidai Oktoba 24, mwaka jana, katika eneo la Mandaka, Kata ya Kilema Kusini, Msaidizi wa Baba Mtakatifu Padri Msafiri alikuwa kwenye ibada iliyofanyika kanisani hapo na alikuwa akigawa vipeperushi vya Mbatia kwa waumini.

Mrema alidai siku ya ibada yeye na Mbatia hakuwakupo kanisani, lakini salamu za mbunge huyo zilisomwa mbele ya waumini na taarifa ya yaliyojiri alipelekewa na watu waliokuwapo pamoja na kipeperushi mojawapo.

Alidai katika jimbo hilo lina makanisa zaidi ya 100 na yote yalipata vipeperushi, isipokuwa moja ambalo huwa anasali lililopo katika Kijiji cha Kiraracha, Kata ya Marangu Magharibi na ndilo eneo ambalo Mbatia alipata kura chache kuliko zote.

Katika kesi hiyo, Mrema anamlalamikia Mbatia, msimamizi wa uchaguzi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali akidai uchaguzi haukuwa huru na wa haki.
TUPE MAONI YAKO HAPO CHINI
[MATUSI HAYARUSIWI]
Share on Google Plus
    Facebook Comment
    Blogger Comment

0 comments:

Post a Comment